Monday, April 13, 2015

Wafanyabiashara wa vitunguu Singida walia na Waganda, Wakenya


Singida. Wafanyabiashara wa vitunguu katika Soko la Misuna, Singida wameiomba Serikali kuwasaka na kuwakamata wafanyabiashara kutoka Kenya na Uganda wanaonunua zao hilo moja kwa moja kutoka kwa wakulima kwa madai kuwa wanawanyonya wakulima na kuikosesha halmashauri mapato.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti juzi, wafanyabiashara hao walidai kuwa baadhi ya madiwani katika maeneo yanayolimwa vitunguu huwasaidia wafanyabiashara hao kununua vitunguu kutoka kwa wakulima badala ya kununua kwenye soko.
Mwenyekiti wa wafanyabiashara hao, Joseph Nadoo alisema mbaya zaidi, wafanyabiashara hao hutumia magunia aina ya neti yenye ujazo mkubwa ukilinganisha na magunia ya kawaida.
“Hawa wafanyabuiashara kutoka Kenya na Uganda wakati mwingine tunaambiwa wananunua vitunguu vikiwa shambani (havijavunwa), huku ni kuwapunja wakulima, lazima Serikali ya Mkoa iliangalie hili badala ya kulifumbia macho,” alisema mmoja wa wafanyabiashara katika Soko la Misuna ambaye alikataa kutajwa jina kwa usalama wake.
Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Faustine Kiyui alisema ofisi yake haina taarifa kama wafanyabiashara hao huwa wanakwenda moja kwa moja kwa wakulima na hutumia magunia yenye ujazo mkubwa.
Alisema watachunguza na wakibaini, hatua zitachukuliwa dhidi yao.
Serikali mkoani hapa kwa miaka mingi, imekuwa ikipiga marufuku wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi kununua vitunguu moja kwa moja kutoka kwa wakulima na badala yake ikiwataka wanunue katika soko maalumu la zao hilo la Mihuna, marufuku ambayo imeshindikana.

No comments:

Post a Comment